Friday, November 4, 2011

Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Wanajumuiya ya Afrika ya Mashariki waishio Marekani

Wana Jumuiya ya Afrika Mashariki wanaoishi Florida Nchini Marekani wameombwa kuendelea kushirikiana pamoja kwa lengo la kutatua matatizo wakati yanapotokea na kuwazunguuka.
Ombi hilo limetolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi Mjini Tallahassee Jimbo la Florida Nchini Marekani baada ya kushiriki katika chakula cha pamoja na Wana Jumuiya hao.
Balozi Seif alisema matatizo mengi yanayowakabili wanaadamu yanashindwa kupatiwa ufumbuzi kutokana na kukosekana kwa ushirikiano wa pamoja.
“ Wana Jumuiya nyinyi ni vyema mkapendana na kushirikiana kwa vile mko mbali na familia zenu mnazozitegemea. ”. Alisema Balozi Seif Al Idi.
Amewataka kufuata Sheria na taratibu zilizowekwa Nchini humo ili kuepuka adhabu inayoweza kuwaletea balaa katika mfumo wa maisha yao ya kila siku.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif amewapongeza wana jumuiya hao wa Afrika Mashariki wanaoishi Florida Marekani kwa uwamuzi wao wa kuunda umoja wao unaosaidia kusukuma mbele maisha na Maendeleo yao.
Hata hivyo amewakumbusha hatma ya maisha yao ya baadaye ambayo inahitaji kufanyiwa maandalizi ya msingi.
Balozi Seif alisema haipendezi kuona mwana Jumuiya anafanya kazi ughaibuni lakini hatma ya maisha yake arudipo nyumbani inavunja moyo.
“ Inakua karaha unarudi ughaibuni na kutaka kuishi kwenye nyumba ya mjomba. Huko ni kujidhalilisha na kujimaliza kimaisha ”. Alitahadhaisha Balozi Seif Ali Iddi.
Umoja wa Wanajumiya ya Afrika Mashariki ulioanzishwa karibu miaka saba iliyopita Umejumuisha pia Wanachama kutoka Mataifa ya Carribean na Nigeria.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar

No comments:

Post a Comment