Sunday, November 6, 2011

100% yafunika Nungwi

Sherehe za maridhiano na umoja wa kitaifa zilizoandaliwa na taasisi ya Swahili Center zinaendelea kwa kasi ambapo kwa Ijumaa iliyopita, vikundi vya Nyota ya Umoja (Maigizo,Nungwi) na Mkota Ngoma (Mkoani, Pemba) vilirindima katika kijiji cha Nungwi, Unguja.
Katika onesho hilo ambalo lilifanyika katika Uwanja wa Skuli ya Nungwi, Wilaya ya Kaskazini A, Mkoa wa Kaskazini Unguja, wapenzi wa fani za sanaa za maonesho kutoka sehemu mbali mabli waliliminika na kujimwaga katika burudani hizo zilizoanza saa 10 alasiri.
Kundi la Maigizo la Nyota ya Umoja, maarufu kwa michezo yao kama vile ‘Dhulma Kafara’ na ‘Masikini naye Mtu’, walitoa burudani safi kupitia mchezo wa ‘Mchelea Mwana Kulia’ uliobeba maudhui ya umuhimu wa ushirikiano wa kuyalinda maadili ya KiZanzibari ndani ya jamii.
Nalo kundi la Mkota Ngoma kutoka Mkoani, walikonga nyoyo za wapenzi wa Ngoma na asili kwa kupiga ngoma zao za Msembwe, Unjunguu na Kumbwaya. Wengi waliohudhiria shehere hizo walivutiwa sana na umahiri wa kundi hilo katika kuzicheza Ngoma hizo.
Katika kuutambulisha mradi huo kwa waliohudhuria onesho hilo, Mkurugenzi Mtendaji wa Swahili Center Bw. Kheri Abdalla Yussuf, aliwajulisha wapenzi hao wa sanaa za utamaduni kuwa dhamira ya mradi huo ni kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa nchini Zanzibar kupitia sanaa za utamaduni zenye burudani na mafunzo kwa jamii yote.
Wakati huo huo, aliyekuwa mgeni rasmi katika onesho hilo, Mhe. Bi Riziki Juma Simai (Mkuu wa Wilaya ya Kasakazi A) aliwataka wananchi wa Nungwi na wote waliohudhuria kuimarisha misingi ya umoja wa kitaifa kwa vitendo.
Mradi wa 100% Zanzibari (tafsiri; Mzanzibari asilimia mia moja) umekuwa ukifanya maonesho katika Mikoa ya Unguja na Pemba kufuatia kambi za kisanii zinazoshirikisha fani za Taarab, Ngoma za Utamaduni na michezo ya Kuigiza. Shangwe hizo zimekuwa zikifanyika kwa awamu katika sehemu mbali mbali ambapo kwa kipindi cha Nov 15-19 zitahamia katika Mkoa wa Mjini Maghribi.
Swahili Performing Arts Center (Kituo cha Sanaa za Maonesho cha Waswahili) ni taasisi ya iliyoanzishwa kwa dhamira ya kuchangia katika maendeleo ya sanaa za maonesho asilia za Zanzibar pamoja na zile za mwambao wa Waswahili kupitia uwezeshaji (wasanii), uzalishaji wa kazi za sanaa, maonesho na ushirikishaji jamii. Dira ya Swahili Center ni kuurejeshea hadhi utambulisho wa utamaduni wa Kiswahili.
Mradi wa 100% Zanzibari umedhaminiwa na Ubalozi wa Norway pamoja na kampuni ya mawasiliano ya Zantel.
Kheiri A.Y. Jumbe
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji

No comments:

Post a Comment