Wednesday, November 14, 2012

Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Dodoma



SMZ: Yasisitiza afya ya uzazi wa pango

Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema kuwa jamii inahitaji kuelimishwa zaidi juu ya umuhimu wa uzazi wa mpango kwa maendeleo ya nchi na kutunza afya ya jamii hasa kwa akina mama na watoto.

Kauli hiyo imetolewa na Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad katika hafla ya uzinduzi wa Ripoti ya Idadi ya Watu Duniani ya mwaka 2012 iliyofanyika katika viwanja vya skuli ya Mkwajuni Mkoa wa Kaskazini Unguja, ambako alimuwakilisha Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohd Shein.

Amesema jamii bado haijatoa umuhimu unaostahiki katika matumizi ya njia za uzazi wa mpango, hali inayopelekea kuwepo kwa ongezeko kubwa la watu ambalo huathiri harakati za maendeleo na afya ya jamii.

“Taarifa zinaonesha kwamba Zanzibar hivi sasa inakadiriwa kuwa na idadi ya watu 1.3 milioni, wanaoongezeka kwa kasi ya asilimia 3.1 kwa mwaka ambapo idadi ya watu katika kila kilomita moja ya mraba imefikia watu 496 mwaka 2011”, ilieleza sehemu ya hotuba hiyo ya Dkt. Shein iliyosomwa na Makamu wa Kwanza wa Rais.

Amefahamisha kuwa bado vifo vya mama wajawazito viko juu duniani lakini vimepungua kwa upande wa Tanzania na Zanzibar hasa kwa kina mama wenye umri mdogo na wanaokabiliwa na tatizo la umaskini.

“Kwa Tanzania katika mwaka 2004/05 idadi ya vifo ilikuwa 578 kwa kila akina mama waja wazito 100,000 na kupungua kidogo hadi kufikia vifo 454 mwaka 2010. Hata hivyo kwa Zanzibar vifo vya akina mama vimepungua kutoka vifo 473 mwaka 2006 hadi vifo 281 mwaka 2011, kwa kila kina mama 100,000 kwa takwimu za hospitali”, alifafanua.

Amesema mafanikio hayo yametokana na juhudi za serikali katika kuimarisha huduma za afya kwa jamii ikiwa ni pamoja na kutoa chanjo za pepopunda na shurua, sambamba na kuimarisha huduma za afya ya uzazi katika hospitali mbali mbali.

Kwa upande wao wawakilishi wa Umoja wa Mataifa wameipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kuona umuhimu wa huduma ya uzazi na kuamua kutoa huduma hiyo bila ya malipo.

Mwakilishi Mkaazi wa Shirika la Idadi ya watu (UNFPA) Tanzania bibi Mariam Khan amesema bado suala la uzazi wa mpango linakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na wanajamii kuona ugumu juu ya matumizi ya njia za uzazi wa mpango.

Amefahamisha kuwa uzazi wa mpango ni muhimu katika kusaidia kukuza kipato cha wanafamilia, sambamba na kuwaendeleza watoto katika makuzi bora, na wito kwa jamii kutoa fursa zinazostahiki kwa akina mama na watoto ili kusaidia harakati za maendeleo kwa jamii.

Waziri wa Afya Mhe. Juma Duni Haji amesema wameamua kufanya uzinduzi huo katika Mkoa wa Kaskazini Unguja, ili kutoa uelewa zaidi kwa wakaazi wa Mkoa huo ambao ni miongoni mwa mikoa inayofanya vibaya katika suala la uzazi wa mpango.

Amesema akinamama na watoto wanahitaji kulindwa kiafya, na kuwataka wazazi kushirikiana katika suala la malezi na makuzi ya watoto.

Mapema akitoa muhtasari wa ripoti hiyo, Katibu Mkuu Wizara ya Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo Khamis Mussa amesema kimsingi ripoti hiyo imeelezea juu ya changamoto, faida na haki za binadamu katika uzazi wa mpango.

Amesema uzazi wa mpango ni miongoni kwa haki za binadamu lakini imeelekezwa zaidi kwenye haki za kifamilia, ili wanafamilia waweze kupanga juu ya idadi na umri wa kupishana kwa watoto, ili kuepuka mimba zisizotarajiwa.

“Inakisiwa kuwa kiasi cha mimba milioni 80 zinapatikana bila ya kutarajiwa duniani, huku nusu ya mimba hizo zikitolewa, jambo ambalo ni hatari nyengine katika uzazi”. Alidokeza Katibu Mkuu huyo.

Hassan Hamad, OMKR.

Friday, November 9, 2012

Dr.Shein ampongeza Obama

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein ametuma salamu za pongezi kufuatia ushindi wa Rais Barack Obama wa Marekani katika Uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo uliofanyika hivi karibuni.
 
Katika salamu zake za pongezi kwa kiongozi huyo wa Marekani ambaye amechaguliwa kwa mara nyengine tena na wananchi wa nchi hiyo kwa kipindi cha pili, Rais Dk. Shein alieleza jinsi alivyopokea kwa furaha ushindi huo pamoja na wananchi wote wa Zanzibar.
 
Salamu hizo za pongezi zilieleza kuwa kwa niaba yake binafsi pamoja na wananchi wa Zanzibar anatuma salamu za pongezi kwa Rais Obama kwa ushindi mkubwa alioupata katika uchaguzi uliofanyika hivi karibuni nchini humo.
 
Aidha, salamu hizo zilieleza kuwa  wananchi wa Marekani wameona umuhimu wa kumuunga mkono Rais Obama na kumrejesha tena madarakani kwa lengo la kuliendeleza na kuliongoza taifa hilo kubwa duniani kwa kipindi cha miaka mine ijayo.
 
Pamoja na hayo, salamu hizo zilieleza kuwa wananchi wa Zanzibar wanaungana na rafiki zao wa Marekani katika kusherehekea ushindi huo uliotokana na uchaguzi mkuu wa hivi karibuni wa Marekani ambao umempa ushindi Rais Obama.
 
Dk. Shein alimtakia uongozi mwema Rais Obama na kutoa salamu za pongezi kwa familia ya Rais Obama akiwemo Mkewe Mama Michelle Obama  na watoto wake wote Malia na Sasha Obama  pamoja na wananchi  wa Marekani ambao wameonesha wazi imani na uaminifu mkubwa walionao katika uongozi wa Rais Obama.
 
Sambamba na hayo, salamu hizo zilieleza kuwa  uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya Zanzibar na Marekani utazidi kuimarika.
 
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.

Balozi wa India akutana na Dr.Shein Ikulu Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameleza haja kwa Serikali ya India kurejesha utamaduni uliokuwa ukifanya miaka ya nyuma wa kuwaleta madaktari bigwa kwa amu hapa Zanzibar hatua ambayo ilisadia sana kuimarisha sekta ya afya na kutoa huduma kwa jamii wakati huo.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Balozi mdogo wa India aliopo Zanzibar Mhe. Pawan Kumar ambaye alifika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha.


Dk. Shein alisema kuwa mnamo miaka ya 1970 hadi mwanzoni mwa miaka ya 1980, India ilikuwa na utaratibu huo wa kutela madaktari bingwa hapa Zanzibar ambao waliweza kufanya kazi zao na kutoa huduma za afya kwa wananchi hatua ambayo ni busara kuanzishwa tena ili kuendeleza kuimarisha sekta ya afya hapa Zanzibar.


Katika maelezo yake Dk. Shein alisema kuwa kuwepo kwa madaktari bigwa hapa nchini kutoka India kutasaida zaidi kuimarisha huduma katika hospitali za Zanzibar hasa hospitali za Wete na Chake kisiwani Pemba ambazo kwa hivi sasa zina upungufu wa madaktari bigwa.


Mbali na hatua hiyo, Dk. Shein alisisitiza umuhimu wa kubadilishana uzoefu na utaalamu kwa madatari wa India na Zanzibar kwa awamu, juhudi ambazo zitasaidia kuipinguzia gharama Serikali ya kupelekea wagonjwa katika hospitali zilizopo nchini humo.
 
Aidha, Dk. Shein alieleza haja ya kuanzisha Mkataba wa Makubaliano juu ya kuimarisha sekta ya afya kati ya India na Zanzibar.

Pia Dk. Shein alimueleza Balozi huyo uhusiano wa siku nyingi katika sanaa ya uimbaji ambao upo kati ya India na Zanzibar hali ambayo ilimpelekea mwimbaji maarufu marehemu Siti Binti Saad kwenda kurikodi katika studio za nchi hiyo nyimbo zake mbali mbali ambazo zilimjengea sifa kubwa duniani.


Kwa upande wa sekta ya kilimo, Dk. Shein alieleza kuwa kutokana na India na Zanzibar kufanana kijiografia kuna umuhimu wa nchi hizo kuendeleza ushirikiano katika sekta hiyo ambayo ni tegemeo kubwa la uchumi wa Zanzibar na wananchi wenyewe.


Dk. Shein alieleza kuwa India ni miongoni mwa nchi zilizopiga hatua katika kufanya utafiti wa kilimo hivyo alieleza haja ya kuimarisha ushirikiano katika sekta hiyo hasa kwa kushirikiana na wataalamu wa Kitengo cha Utafiti wa Kilimo kiliopo Kizimbani.


Kutokana na Balozi huyo kuwa mpya katika mazingira ya Zanzibar Dk. Shein alimshauri kutembelea katika maeneo ya kilimo cha mpunga ili aweze kuona uhalisia na hatua zilizofikiwa na wananchi pamoja na juhudi za serikali za uimarishaji wa sekta hiyo.


Akieleza juu ya zao la karafuu, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa kwa vile India wana historia ya ununuzi na utumiaji wa karafuu kutoka Zanzibar hivyo ipo haja kya kuimarisha ushirikiano wa kibiashara katika zao hilo.


Pia, Dk. Shein alipongeza maendeleo makubwa yaliofikiwa na India katika sekta ya elimu na kueleza kuwa nchi hiyo hivi sasa imekuwa ikitoa mafunzo mbali mbali kwa wanafunzi kutoka nchi tofauti duniani na kueleza kufarajika kwake kutokana na wanafunzi wengi wanaotoka Zanzibar na kwenda nchini humo kusoma fani mbali mbali.


Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendeleza ushirikiano katika sekta hiyo ya elimu huku akipongeza juhudi za India za kutaka kuanzisha Chuo cha Mafunzo ya Amali huko kisiwani Pemba pamoja na juhudi za kuanzisha mradi wa kutoa mafunzo kwa watoto wa kike vijijini.


Nae Balozi huyo mdogo wa India aliopo hapa Zanzibar Mhe. Pawan Kumar alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake itaendeleza uhusiano na ushirikiano uliopo ambao ni wa muda mrefu na umekuwa na historia kubwa.


Balozi Pawan Kumar alieleza kupokea rai zilizotolewa na Dk. Shein katika kuimarisha sekta ya afya nchini pamoja kuahidi kuzifanyia kazi ipasavyo.


Alieleza kuwa kwa upande wa sekta ya Afya India itaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika sekta hiyo ikiwa ni pamoja na kuendelea kutoa nafasi za masomo kwa madaktari wazalendo. Aidha, Balozi huyo alieleza kuwa mbali ya nafasi za masomo kwa madaktari wazalendo pia, nchi hiyo itaendelea kutoa nafasi za masomo katika fani nyengine tofauti.
 

Balozi Pawan Kumar pia, alibainisha kuendeleza ushirikiano katika kuimarisha nishati pamoja na juhudi za kujikinga na maafa.

Pamoja na hayo, Balozi huyo alimueleza Dk. Shein azma ya India ya kujenga Chuo cha Amali kisiwani Pemba, hatua ambayo itasaidia katika kuimarisha sekta ya ajira na kutoa utaalamu kwa wananchi.
 

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.