Tuesday, August 20, 2013

Dk.Shein apongeza PBZ

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesifu hatua zilizochukuliwa katika kuiimarisha Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) ikiwa ni pamoja na utoaji mikopo kwa wajasiriamali na kujiunga na mitandao mbali mbali kwa ajili ya kutoa huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokutana na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugrnzi wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), na kufanya nao mazungumzo huko Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Shein alieleza kuwa mafanikio makubwa yameweza kupatikana kutokana na uongozi thabiti wa benki hiyo sambamba na umakini wa vionghozi wa Serikali kuu.

Alieleza matumaini yake makubwa katika benki hiyo kutokana na na hatua mbali mbali inazozichukua katika kujiimarisha hali ambayo itaimarisha uchumi na maendeleo ya Zanzibar na watu wake.

Kwa upande wa kujiunga na mitandao mbali mbali kwa ajili ya kutoa huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora, Dk. Shein alipongeza hatua hiyo na kusema kuwa italeta maendeleo makubwa na kuweza kutimiza azma ya serikali anayoiongoza.

Aliwataka wajumbe hao kutorudi nyuma na badala yake waendelee na juhudi zao hizo huku akieleza kuwa serikali imedhamiria kuwasaidia wajasiariamali na ndio maana ina mpango kabambe wa kuanzisha Mfuko maalum utakaowasaidia huku akipongeza azma ya PBZ ya kuwasaidia wajasiriamali.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza azma ya Serikali katika kuwasaidia wakulima kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa chakula na tayari imeshaanza kupunguza ruzuku pembejeo za kilimo zikiwemo matreka, dawa, mbegu, mbolea na kusisitiza mpango wa Serikali wa kununua matrekta 20 mwaka huu.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alipongeza juhudi za PBZ katika kuanzisha huduma za kibenki kwa njia ya mitandao ya simu za mkononi pamoja na internet, huduma ambayo itarahisiha upatikanaji wa huduma zake kwa urahisi zaidi.

Nao Wajumbe wa Bodi hiyo ya Wakurugenzi wa PBZ, walieleza maendeleo yaliopatikana na Benki hiyo baada ya uimarishaji wake na kueleza ukuaji wa amana za wateja na rasiliamli sambamba na ukuaji wa kikopo kwa wateja.

Bodi hiyo ilieleza kuwa PBZ imeweza jinsi ilivyofanyia matengenezo matawi yake ikiwa ni pamoja na kujenga jengo jipya la ChakeChake na kuweka mtandao wa ATM ili kupunguza foleni.

Aidha, Bodi hiyo ilieleza kuwa tayari imeshafungua matawi kutoka matawi matatu hadi matawi tisa na vituo vine katika sehemu mbali mbali, kuanzia mwaka 2010 hadi 2012.

Kwa upande wa huduma za benki ya Kiislamu uongozi huo ulieleza kuwa tayari PBZ imeshafungua matawi matatu ya huduma za benki ya Kiislamu, na tawi la nne pamoja na Makao Makuu yake yatafunguliwa hivi karibuni katika jengo la ZIC.

Sambamba na hayo uongozi huo ulieleza juhudi ilizozichukua katika kuanzisha huduma za ATM, kuanzisha huduma za kibenki kwa njia ya simu za mkononi pamoja na internet, azma ya kutoa mikopo ya nyumba pamoja na kuanzisha huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.

Wanahaari pia wanajukumu la kutathimini kile wanachota kukifanyia kazi


Imeelezwa kuwa wanahabari kufanya kazi kwa uhakika na kutasmini kile ambacho anakitenda ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima. 

Tuesday, August 6, 2013

Dk.Sheni aungana na wananchi katika futari

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein jana aliungana na wananchi pamoja na viongozi mbali mbali wa Mkoa wa Mjini Magharibi katika futari maalum aliyowaandalia huko Ikulu mjini Zanzibar.

Akitoa shukurani kwa niaba ya Rais wa Zanzibar, Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein pamoja na wafanyakazi wa Ikulu, Waziri wa Nchi Afisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Mwinyihaji Makame alitoa shukurani hizo kwa wananchi kwa kuitikio mwaliko huo wa Rais.

Dk. Mwinyihaji Makame aliendelea kutoa shukurani hizo kwa wananchi kwa niaba kufuatia wananchi wengi kujitokeza katika futari hiyo maalum aliyoiandaa Rais.

Aidha, katika shukurani zake hizo Dk. Mwinyihaji Makame aliwapongeza wananchi wa Zanzibar kwa kuendelea kuishi kwa upendo ikiwa ni pamoja na kudumisha amani, masikilizano na maelewano miongoni mwao.

Alisema kuwa hatua hiyo imepelekea wananchi kuweza kufanya ibada zao mbali mbali katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kwa amani na utulivu mkubwa.

Pamoja na hayo, Dk. Mwinyihaji Makame alisisitiza kuwa umoja, mshikamano, upendo na masikilizano miongoni mwa wananchi wa Zanzibar ndio msingi mkubwa wa maendeleo huku akitoa shukurani kwa MwenyeziMungu kwa kuendelea kuijalia Zanzibar kuwa na mazao tofauti katika msimu huu wa kilimo.

Wananchi pamoja na Viongozi mbali mbali wa dini, vyama na Serikali walihudhuria akiwemo Makamo wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais Mstaafu wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume, Waziri Kiongozi Mstaafu wa Zanzibar Ramadhani Haji Faki, Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabih, Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji, Mabalozi wadogo wa nchi za nje waliopo Zanzibar na wengineo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.

Sunday, July 21, 2013

Dk.Shein afutarisha Pemba


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein jana ameungana na wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba katika futari maalum aliyowaandalia huko Ikulu ndogo ya Chake.

Akitoa shukurani kwa niaba ya Mhe. Rais Alhaj Dk. Shein, Mkuu wa Mkoa wa Kusini Pemba Mhe. Juma Kasim Tindwa alitoa shukurani kwa wananchi wote waliokubali mwaliko na kuhudhuria katika futari hiyo waliyoandaliwa na Rais ambayo imeonesha upendo mkubwa kwao.

Katika maelezo yake, Mkuu wa Mkoa huyo aliwasihi Masheikh katika Mkoa huo kuendelea kuhubiri amani na utulivu kwani hiyo ndio ngao pekee ya kujiletea maendeleo endelevu na kuishi katika maisha ya upendo.

Nao wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba wakitoa shukurani zao ambazo kwa niaba zilitolewa na Sheikh Mohammed Khamis na kueleza furaha za wananchi hao kwa kufutari pamoja na kiongozi wao wa nchi.

Katika maelezo yake Sheikh Khamis alitoa pongezi kwa Alhaj Dk. Shein kwa juhudi zake za kuwa karibu na wananchi katika shughuli mbali mbali za kimaendeleo zikiwemo za kidini.

Wananchi hao walieleza kuwa katika uongozi wa Rais Dk. Shein wameweza kuona uongozi wa uadilifu anaoufanya pamoja na kutumia busara kubwa na unyenyekevu katika kuongoza nchi.

“Tumeweza kuona uadilifu wako mkubwa katika kuongoza nchi ikiwa ni pamoja na kushiriki katika shughuli mbali mbali za kidini zikiwemo ufunguzi wa misikiti katika maeneo mbali mbali”,alisema Sheikh Mohammed Suleiman.

Pamoja na hayo, wananchi hao walimtakia uongozi mwema kiongozi huyo na kuiombea nchi iendelee kuwa na amani na utulivu na kuwasisitiza wananchi kuendelea kushirikiana pamoja.

Rajab Mkasaba, Pemba.

Tuesday, July 16, 2013

Dk.Shein atowa salama za rambi rambi kwa mkuu wa majeshi Tz

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, pamoja na wananchi wa Zanzibar wamepata mshtuko na huzuni kubwa kwa vifo vya wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi wa Watanzania walioshambuliwa na kuuawa wakati walipokuwa wakilinda amani katika eneo la Darfur, nchini Sudan.

Dk. Shein ameelezea kusikitishwa kwake na vifo hivyo na kueleza kuwa inasikitisha zaidi kuwa wanajeshi hao wamekufa wakiwa katika kazi ya kulinda amani nchini humo na kueleza kuwa wao ni mashujaa na wamekufa kishujaa.


Hayo yalielezwa katika salamu zake za rambi rambi alizotuma Dk. Shein kwa Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananachi wa Tanzania, Jenerali Davis Adolf Mwamunyange pamoja na wanajeshi wote, pia, salamu hizo zilitoa pole kwa familia za wafiwa.


Aidha, salamu hizo alizozituma Dk. Shein zilieleza kuwa huu ni msiba wa Taifa lote na wananchi wote wa Zanzibar wanaungana pamoja katika kuomboleza msiba huo.


“Tunatoa pole na tunamuomba MwenyeziMungu aziweke pahala pema peponi roho za mashujaa hao, vile vile tunawatakia nafuu ya haraka majeruhi wote wa tukio hilo”.


Alisisitiza Dk. Shein “ Mwenyezi Mungu akupeni moyo wa subira na ustahamilivu katika kipindi hiki cha msiba mkubwa”. zilieleza salamu hizo za rambirambi


Dk. Shein pamoja na wananchi wa Zanzibar wanaungana na Watanzania wenzao kuwaombea wale wote walioumia katika tukio hilo ili waweze kupona kwa haraka na kuendelea na majukumu yao ya ulinzi wa amani.


Vijana saba wa Jeshi la Wananachi wa Tanzania waliuawa baada ya kushambuliwa na waasi wa Sudan na wengine walijeruhiwa.


Wanajeshi hao wa Tanzania waliopoteza maisha yao pamoja na wale walioumia walikuwa ni sehemu ya askari 37 na ofisa mmoja ambao walikuwa wanasindikiza msafara wa waangalizi wa kijeshi katika eneo la Darfur.


Katika suala la ulinzi wa amani katika eneo hilo la Darfur, Wanajeshi kutoka Tanzania wamekuwa wakifanya kazi nzuri ya ulinzi tokea pale Tanzania ilipoanza kuchangia walinzi katika eneo hilo mnamo mwaka 2007, ambapo vijana hao waliouawa ni miongoni mwa vijana waliokwenda nchini humo Februari mwaka huu.


Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Dk.Shein aipongeza UNICEF

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amelipongeza Shirika la Umoja wa Mataifa linalowahudumia Watoto (UNICEF), kwa juhudi zake za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Mwakilishi wa UNICEF nchini Tanzania Dk. Jama Gulaid, aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kumtambulisha Mama Francesca Moranditi atakayefanya kazi za Shirika hilo katika ofisi ya Zanzibar.


Katika maelezo yake Dk. Shein aliueleza uongozi huo wa UNICEF nchini Tanzaia kuwa Shirika hilo limekuwa na historia kubwa na mashirikiano na Zanzibar kwa muda mrefu.


Alieleza kuwa UNICEF imeweza kushirikiana vyema na Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo pamoja na huduma za kijamii ikiwa ni pamoja na kuimarisha sekta ya afya, elimu pamoja na kuwasaidia na kuwajengea uwezo akina mama na watoto.


Dk. Shein katika maelezo yake alisema kuwa Shirika hilo limeweza kutoa msaada wake mkubwa kwa kushirikiana na Shirika la Afya duniani (WHO), katika kuimarisha sekta ya fya hapa nchini.


Alisisitiza kuwa Zanzibar imeweza kujiweka katika nafasi nzuri katika kufikia malengo ya Milenia katika sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya afya kwa kuweza kuungwa mkono na washirika wa maendeleo likiwemo shirika hilo la UNICEF.


“ Kwa upande wangu binafsi pamoja na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar tunatoa pongezi kwa UNICEF kwa kuendeleza ushirikiano wake kwetu na kuendelea kutuunga mkono kwa muda mrefu”,alisema Dk. Shein.


Aidha, Dk. Shein alisema kuwa kupungua vifo vya akina mama na watoto hapa nchini ni miongoni mwa mafanikio makubwa yaliopatikana na Setrikali ya Mapinduzi Zanzibar.


Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumkaribisha Mama Morandini hapa Zanzibar na kumuhakikishia kuwa mashirikiano makubwa atayapata kutoka kwa viongozi wa Serikali na wananchi wa Zanzibar kutokana na ukarimu wao na utamaduni wao wa kupenda wageni.


Mapema katika mazungumzo yake, Dk. Jama Gulaid alimueleza Dk. Shein kuwa Zanzibar imepata mafanikio makubwa katika kuimarisha sekta zake za maendeleo na kutoa pongezi zake kwa kuendelea kuwaenzi na kuwatunza watoto.


Alisema kuwa mbali na juhudi hizo Zanzibar imeweza kupata mafanikio katika kupunguza vifo vya akina mama na watoto pamoja na kupambana na Malaria hatua ambayo imeipa sifa Zanzibar ndani na nje ya Bara la Afrika.


Dk. Gulaid alieleza kuwa mabadiliko makubwa yameweza kutokea hapa nchini katika kuhakisha watoto wanapata haki zao za msingi pamoja na mahitaji yao muhimu juhudi ambazo zinaendelea kufanywa na Serikali anayoiongoza Dk. Shein.


Kutoka na juhudi hizo Mwakilishi huyo wa UNICEF nchini Tanzania alimuhakikishia Dk. Shein kuwa Shirika hilo litaendelea kutoa ushirikiano wake na kuendelea kuiunga mkono Zanzibar ili iweze kupata mafanikio zaidi.


Sambamba na hayo, Dk. Gulaid alimueleza Dk. Shein kuwa UNICEF itandelea kuwajengea uwezo wafanyakazi wake pamoja na kuziimarisha ofisi zake zote zilizopo hapa nchini Tanzania ili ziweze kufanya kazi kwa ufanisi zaidi.


Nae Mama Francesca Morandini alitoa pongezi na shukurani kwa Dk. Shein kutokana na kumkaribisha Zanzibar na kumuahidi kuwa UNICEF inathamini na kutambua juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya uongozi wa Dk. Shein hasa katika kuwajali watoto.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.