Wednesday, October 17, 2012

Dk.Shein awaapisha viongozi wapya

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein leo amewaapisha viongozi na watendaji katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kufuatia uteuzi alioufanya hivi karibuni.
 
Katika hafla hiyo iliyofanyika Ikulu mjini Zanzibar na kuhudhuriwa na viongozi mbali mbali Dk. Shein alimuapisha Mhe. Shawana Bukheti Hassan ambaye ameapishwa kuwa  Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi na Waziri asiekuwa na Wizara Maalum.
 
Miongoni mwa viongozi waliohudhuria ni Makamu wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Rais Mhe. Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Mhe. Pandu Ameir Kificho, Waziri wa Nchi Afisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Mwinyihaji Makame
 
Wengine ni Waziri wa Nchi Afisi ya Makamu wa Pili wa Rais Mhe. Mohammed Aboud, Waziri wa Ardhi, Makaazi, Maji na Nishati Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban, Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdillahi Jihad Hassan, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Mhe. Abdalla Mwinyi Khamis, Meya wa Manispaa ya Mji wa Zanzibar, Mstahiki Khatib Abdulrahman Khatib pamoja na viongozi wengine.
 
Wakati huo huo, Dk. Shein amewaapisha viongozi wengine akiwemo Naibu Waziri wa Kilimo na Maliasili Mhe. Mtumwa Kheir Mbarak pamoja na Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Mohamed Said Mohamed.
 
Viongozi wengine walioapishwa katika hafla hiyo ni Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Bwana Tahir M. Abdalla pamoja na Bwana Mustafa Aboud Jumbe ambaye ambae ameapishwa kuwa Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano.
 
Pia, Dk. Shein amemuapisha Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi anaeshughulikia Idara Maalum za SMZ, CDR Julius Nalimy Maziku pamoja na Naibu Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais (Fedha, Uchumi na Mipango ya Maendeleo) Bwana Juma Ameir Hafidh.
 
Hapo juzi, Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein alifanya mabadiliko ya viongozi na watendaji wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kutumia uwezo aliopewa chini ya vifungu vya  Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ambapo pia, alifuta rasmi uteuzi wa Mhe. Mansoor Yussuf Himid kuwa Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi kuanzia Oktoba 15 mwaka huu na Mhe. Shawana Bukheti Hassan aliteuliwa kuwa Mjumbe wa Baraza la Mapinduzi.
Rajab Mkasaba, Ikulu