Tuesday, August 20, 2013

Dk.Shein apongeza PBZ

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesifu hatua zilizochukuliwa katika kuiimarisha Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) ikiwa ni pamoja na utoaji mikopo kwa wajasiriamali na kujiunga na mitandao mbali mbali kwa ajili ya kutoa huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora.

Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokutana na Wajumbe wa Bodi ya Wakurugrnzi wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), na kufanya nao mazungumzo huko Ikulu mjini Zanzibar.

Katika maelezo yake Dk. Shein alieleza kuwa mafanikio makubwa yameweza kupatikana kutokana na uongozi thabiti wa benki hiyo sambamba na umakini wa vionghozi wa Serikali kuu.

Alieleza matumaini yake makubwa katika benki hiyo kutokana na na hatua mbali mbali inazozichukua katika kujiimarisha hali ambayo itaimarisha uchumi na maendeleo ya Zanzibar na watu wake.

Kwa upande wa kujiunga na mitandao mbali mbali kwa ajili ya kutoa huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora, Dk. Shein alipongeza hatua hiyo na kusema kuwa italeta maendeleo makubwa na kuweza kutimiza azma ya serikali anayoiongoza.

Aliwataka wajumbe hao kutorudi nyuma na badala yake waendelee na juhudi zao hizo huku akieleza kuwa serikali imedhamiria kuwasaidia wajasiariamali na ndio maana ina mpango kabambe wa kuanzisha Mfuko maalum utakaowasaidia huku akipongeza azma ya PBZ ya kuwasaidia wajasiriamali.

Sambamba na hayo, Dk. Shein alieleza azma ya Serikali katika kuwasaidia wakulima kwa lengo la kuongeza uzalishaji wa chakula na tayari imeshaanza kupunguza ruzuku pembejeo za kilimo zikiwemo matreka, dawa, mbegu, mbolea na kusisitiza mpango wa Serikali wa kununua matrekta 20 mwaka huu.

Pamoja na hayo, Dk. Shein alipongeza juhudi za PBZ katika kuanzisha huduma za kibenki kwa njia ya mitandao ya simu za mkononi pamoja na internet, huduma ambayo itarahisiha upatikanaji wa huduma zake kwa urahisi zaidi.

Nao Wajumbe wa Bodi hiyo ya Wakurugenzi wa PBZ, walieleza maendeleo yaliopatikana na Benki hiyo baada ya uimarishaji wake na kueleza ukuaji wa amana za wateja na rasiliamli sambamba na ukuaji wa kikopo kwa wateja.

Bodi hiyo ilieleza kuwa PBZ imeweza jinsi ilivyofanyia matengenezo matawi yake ikiwa ni pamoja na kujenga jengo jipya la ChakeChake na kuweka mtandao wa ATM ili kupunguza foleni.

Aidha, Bodi hiyo ilieleza kuwa tayari imeshafungua matawi kutoka matawi matatu hadi matawi tisa na vituo vine katika sehemu mbali mbali, kuanzia mwaka 2010 hadi 2012.

Kwa upande wa huduma za benki ya Kiislamu uongozi huo ulieleza kuwa tayari PBZ imeshafungua matawi matatu ya huduma za benki ya Kiislamu, na tawi la nne pamoja na Makao Makuu yake yatafunguliwa hivi karibuni katika jengo la ZIC.

Sambamba na hayo uongozi huo ulieleza juhudi ilizozichukua katika kuanzisha huduma za ATM, kuanzisha huduma za kibenki kwa njia ya simu za mkononi pamoja na internet, azma ya kutoa mikopo ya nyumba pamoja na kuanzisha huduma za kutuma fedha kwa wana Diaspora.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.

Wanahaari pia wanajukumu la kutathimini kile wanachota kukifanyia kazi


Imeelezwa kuwa wanahabari kufanya kazi kwa uhakika na kutasmini kile ambacho anakitenda ili kuepuka migogoro isiyo ya lazima. 

Tuesday, August 6, 2013

Dk.Sheni aungana na wananchi katika futari

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein jana aliungana na wananchi pamoja na viongozi mbali mbali wa Mkoa wa Mjini Magharibi katika futari maalum aliyowaandalia huko Ikulu mjini Zanzibar.

Akitoa shukurani kwa niaba ya Rais wa Zanzibar, Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein pamoja na wafanyakazi wa Ikulu, Waziri wa Nchi Afisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Mwinyihaji Makame alitoa shukurani hizo kwa wananchi kwa kuitikio mwaliko huo wa Rais.

Dk. Mwinyihaji Makame aliendelea kutoa shukurani hizo kwa wananchi kwa niaba kufuatia wananchi wengi kujitokeza katika futari hiyo maalum aliyoiandaa Rais.

Aidha, katika shukurani zake hizo Dk. Mwinyihaji Makame aliwapongeza wananchi wa Zanzibar kwa kuendelea kuishi kwa upendo ikiwa ni pamoja na kudumisha amani, masikilizano na maelewano miongoni mwao.

Alisema kuwa hatua hiyo imepelekea wananchi kuweza kufanya ibada zao mbali mbali katika mwezi huu mtukufu wa Ramadhani kwa amani na utulivu mkubwa.

Pamoja na hayo, Dk. Mwinyihaji Makame alisisitiza kuwa umoja, mshikamano, upendo na masikilizano miongoni mwa wananchi wa Zanzibar ndio msingi mkubwa wa maendeleo huku akitoa shukurani kwa MwenyeziMungu kwa kuendelea kuijalia Zanzibar kuwa na mazao tofauti katika msimu huu wa kilimo.

Wananchi pamoja na Viongozi mbali mbali wa dini, vyama na Serikali walihudhuria akiwemo Makamo wa Kwanza wa Rais Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Pili wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais Mstaafu wa Zanzibar Dk. Amani Abeid Karume, Waziri Kiongozi Mstaafu wa Zanzibar Ramadhani Haji Faki, Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kabih, Kadhi Mkuu wa Zanzibar Sheikh Khamis Haji, Mabalozi wadogo wa nchi za nje waliopo Zanzibar na wengineo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar.